Sunday, August 26, 2012

DC GEITA AHAMASISHA SENSA,KUUPOKEA MWENGE WA UHURU



Mangochie alieshika bomba
Na Mwandishi wetu
MKUU wa Wilaya ya Geita, Omari Manzie Mangochie amewaasa wananchi wa jimbo hilo kutoa ushirikiano kwa makarani wa sensa, iliyoanza usiku wa kuamkia leo nchini kote.
Akizungumza kwa njia ya simu , Mangochie alisema kuwa, tayari maofisa mbalimbali wa Sensa wamejipanga kutekeleza majukumu yao ndani ya Wilaya hiyo na kutaka ushirikiano wa kutosha huku akiwaasa kuachana na vitendo vya kuchanganya mambo ya siasa, dini na mambo ya msingi.
“Tunaomba ushirikiano  wa kutosha kwa wananchi wa Geita ilikuwasaidia makarani wa sensa watakaopita sehemu mbalimbali na kupata maelezo ya kila mwananchi, na pia suala hili si la siasa wala dini ni la maendeleo yetu sote” alisema Mangochie.
Mangochie pia alisema kuwa Wilaya yake inatarajia kupokea Mwenge wa Uhuru ambao utazindua miradi 15, itakayogharimu kiasi cha Milioni 836.
“Tunatarajia kupokea Mwenge wa Uhuru kesho  na utazunguka Wilayani  na kuzindua miradi ya 15, yenye thamani ya zaidi ya milioni 836,  hii pia utakua hamasa kwa zoezi zima la kuhamasisha sensa ya makazi na watu” alisema Mangochie.
Aidha, Mangochie aliwataka wananchi kuepuka mambo ya misuguano kutoka kwa wananchi wanaopitia njia za kisiasa kwani zitaweza kuleta chuki na baadala yake wawapuuze.
Mwenge huo unatarajiwa kuingia Mkoa huo mpya wa Geita, katika  Wilaya ya Geita ukitokea Sengerema, Ambapo utazunguka kwa siku hiyo moja na kisha kuingia kwenye Wilaya zingine mpya za Mbogwe, Nyang’wale, Bukombwe na kisha Chato.